Saturday, January 5, 2013

Waziri ashikwa na butwaa baada ya ndege kuuzwa kwa sh. laki 5


Cessna 185 1974-1991
Cessna 185



WAZIRI wa Kilimo, Chakula na Ushirika,Mhandisi Christopher Chiza jana alishikwa na butwaa, pale alipopewa taarifa ya kuuzwa ndege tatu za Serikali, ambazo zilikuwa katika Kituo cha Kilimo Anga kwa kiasi cha Sh500,000 kwa kila moja.

Ndege hizo, tatu  zilikuwa zikitumika katika udhibiti wa wadudu waharibifu wa mazao .
Akisoma taarifa ya kituo hicho mbele ya Waziri Chiza, Mhandisi Mkuu wa Ndege wa kituo hicho,Gideon Mugusi,alizitaja ndege hizo kuwa ni 5H-MRN, Cessna 185 nyingine ni 5H-MRF, Cessna 185 na nyingine aina ya  5H-MRP piper Super Cub ambazo zilianguka katika vipindi tofauti.



“Ndege zote tatu ziliharibika lakini Shirika la Bima la Taifa(NIC), walilipa Serikali kupitia katibu mkuu wa Wizara ya Kilimo, kulingana na viwango vya bima vilivyokuwa vikilipwa na wizara”alisema  Mugusi.

Hata hivyo alisema tangu kuanguka na kuuzwa kwa ndege hizo,shughuli za  kituo hicho, Kimekuwa zikidorora  kwani marobani karibu wote wameondoka na kituo kimebaki na ndege moja tu ambayo pia ni mbovu na kibali cha kuruka angani kimekwisha.

Alisema kwa sasa kutokana na kukosekana kwa ndege, gharama za uendeshaji wa shughuli za kituo zimekuwa  ni kubwa mno kwani wanalazimika kukodisha  helikopta na gharama zake zimekuwa zikipanda mwaka hadi mwaka.
Waziri aja juu:

Kutokana na maelezo hayo, waziri Chiza alikuja juu na kuhoji iweje ndege hizo, ziuzwe kwa Sh 500,000 kila moja.
zinaendelea kufanyakazi na zinamilikiwa na nani,”alisema Chiza.

Waziri huyo, pia alihoji iwapo ndege hizo, zilifutwa kwenye orodha ya kumbukumbu za Serikali kama hazifai kwa matumizi pia kama ufutwaji wake ulifuata sheria na kanuni za Serikali.
“Leo sikuja kukamata mchawi, ila mimi binafsi nitafuatilia ili kuona kama sheria zilifuatwa au kama ndege zimeuzwa bila kufuata sheria” alisema Chiza.

Awali alisema Serikali ina mpango wa kufufua kitengo hicho na kwa kuanzia tayari  imetoa fedha za kununua ndege moja.
“Naagiza mfanye mchakato haraka wa kununua ndege hii, hatutaki tena ukiritimba  kwani nia ya Serikali ni kufufua kituo hiki,”alisema Chiza.

Alisema ,kituo hicho  ndiyo pekee katika nchi za Afrika ya Mashariki chenye uwezo wa kutoa huduma hiyo ya kilimo anga na kama ndege zikianza kufanya kazi, basi zitaweza kukodiwa na nchi jirani.

Kituo cha Kilimo Anga kilianzishwa na wizara ya kilimo ,ikishirikiana na Umoja wa Mataifa kupitia Shirika la UNDP na FAO mnamo mwaka 1979 na lengo kubwa lilikuwa ni kuimarisha utoaji huduma katika sekta ya kilimo katika kupambana na visumbufu vya mimea wahamao(migratory pest control).
Enhanced by Zemanta

No comments: