Tuesday, September 3, 2013

UVCCM kimenuka wataka kumpindua mwenyekiti wao

Mwenyekiti wa UVCCM Sadifa Juma Khamis kushoto aliyesimama

Mvutano mkubwa umeibuka ndani ya Jumuiya ya Vijana ya Chama cha Mapinduzi (UVCCM), kutokana na baadhi ya wajumbe wa Baraza Kuu la umoja huo kudhamiria kumng’oa madarakani mwenyekiti wao, Sadifa Juma Khamis.
Mgogoro huo ulisababisha kikao cha Baraza Kuu kilichokuwa kikifanyika Zanzibar juzi, ambacho mgeni rasmi alikuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Balozi Seif Ali Iddi kutofikia mwisho kutokana na baadhi ya wajumbe kumtaka Sadifa na Kamati yake ya Utekelezaji kutoka nje ili wajadiliwe kwa kukiuka kanuni.
Sadifa anadaiwa kukiuka Ibara ya 91 ya toleo la nane la Kanuni za UVCCM kwa kutangaza uteuzi wa wakuu wa idara tatu za umoja huo, kabla ya kuundwa kwa Kamati ya Utekelezaji ambayo kimsingi alipaswa kushirikiana nayo kuwateua, kabla ya kuidhinishwa na baraza kuu.
Habari kutoka katika mkutano huo uliofanyika katika Ofisi ya CCM, Kisiwandui zinasema Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana ndiye aliyeokoa jahazi baada ya kuingilia kati mvutano baina ya baadhi ya wajumbe na Sadifa.
Inaelezwa pia kuwa Katibu Mkuu mpya wa UVCCM, Sixtus Mapunda naye alionja chungu ya mgogoro huo pale alipopingwa vikali na wajumbe, alipojaribu kumtetea mwenyekiti wake.
Hata hivyo, Sadifa na Mapunda kwa nyakati tofauti jana walisema kuwa mkutano huo ulimalizika bila tatizo na ulikuwa na ajenda moja tu ya kumthibitisha Katibu Mkuu jambo ambalo lilifanyika kama ilivyokuwa imepangwa.
“Kwa mujibu wa kanuni, mwenyekiti ndiye mwenye mamlaka ya kufungua na kufunga kikao na vyote hivyo tulifanya, hakuna kikao kilichovunjika,” alisema Sadifa.
Alipotakiwa kueleza kuhusu kanuni anayodaiwa kuivunja, alikataa kuzungumzia suala hilo akitaka kwanza mwandishi amwambie chanzo chake cha habari.
“Nani huyo aliyetaka nitoke, wewe nisikilize, kuna watu ambao wanajua kabisa unataka kuzungumza nini hata kabla hujasema na mmoja wa watu hao ni Sadifa kwa hiyo nilishajua kabisa ni nini unataka,” alisema Sadifa na baada mwandishi kuendelea kumuuliza maswali alikata simu.
Kwa upande wake, Mapunda alisema: “Mkutano ulifanyika na kumalizika kama ulivyokuwa umepangwa. Ule ulikuwa ni mkutano maalumu na ulikuwa na ajenda moja tu, mwenyekiti aliufungua na kuufunga kama ilivyokuwa imepangwa. Ajenda ilikuwa ni kunithibitisha mimi tu (kuwa katibu wa UVCCM) na baada ya hilo kufanyika nilikaribishwa na mimi nikazungumza na nikamaliza”.

Sorce: Mwananchi

No comments: