Sunday, July 1, 2012

Hali tete: Dk. Ulimboka apelekwa nje ya nchi


Bofya hapa chini usikie alichosema Dk Ulimboka muda mfupi baada kuokotwa akiwa amejeruhiwa vibaya baada ya kuteswa 


  
Fedha za matibabu zachangwa na madaktari

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk Steven Ulimboka amesafirishwa kwenda nje ya nchi kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi.Kusafirishwa kwake kunafuatia hatua ya jopo la madaktari waliokuwa wakimhudumia, kueleza mabadiliko ya hali ya afya yake, yaliyosababisha figo kushindwa kufanya kazi, hali iliyolazimu pamoja na matibabu mengine, kwenda   kusafishwa damu.

Ingawa madaktari hao wamekataa kuweka wazi nchi anayopelekwa, kuna taarifa kwamba huenda amesafirishwa kwenda nchini Afrika Kusini.



Katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili (Moi) jana makundi mbalimbali ya watu yalifurika wakiwamo wanaharakati na ndugu wa Dk Ulimboka,  waliofika kwa lengo la kumsindikiza Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Watu hao waliofika hospitalini hapo kuanzia asubuhi, waliendelea kubaki  eneo hilo hadi saa 6:45 mchana msafara ulipoanza.

Dk Ulimboka alisafirishwa kwa gari la kubebea wagonjwa la kampuni ya AAR. Alipofika uwanjani, alisafirishwa kwa  ndege ya kukodi ya Shirika la Ndege la Afrika Kusini, akisindikizwa na watu watatu.

Usiri safari ya Dk Ulimboka

Mapema jana asubuhi, taarifa za kusafirishwa kwake zilizagaa, lakini hapakuwa na mtu wa kuthibitisha safari hiyo na namna atakavyosafiri.

Katika safari hiyo, Dk Ulimboka amesindikizwa na  Dk Pascal Lugajo, kaka yake, Dk Hobakile Ulimboka na mke wake,  Dk Judith Mzovela.

Madaktari watoa tamko

Baada ya Ulimboka kusafirishwa, madaktari walilaani kitendo cha kutekwa na kupigwa mwenzao na kuitaka Serikali itoe tamko juu ya usalama wao.

Katibu wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk Edwan Chitage aliwaambia waandishi wa habari kuwa tukio hilo na vitisho vya kufukuzwa kazi wanataaluma hao kunakofanywa na Serikali, kumezua  hofu kwa  madaktari wote nchini.

“Tunaamini Serikali inawajibika kwa watu wake, kwa hali ilivyo sasa madaktari wapo kwenye hofu kubwa, tunataka itoe tamko juu ya usalama wa madaktari,” alisema Dk Chitage.

Akizungumzia hali ya Dk Ulimboka, alisema imekuwa ikibadilika mara kwa mara hali ambayo imesababisha kumpeleka nje ya nchi kwa matibabu zaidi .

Chitage alisema kama Serikali ingekuwa na nia ya kuboresha huduma hospitalini hapo ingeweza kununua mashine ya CT Scan ambayo alisema bei yake ni sawa na Toyota ‘Shangingi’ moja.

Kwa upande wao wanaharakati wa haki za binadamu, jana walifika Uwanja wa Ndege wakiwa na mabango yenye ujumbe tofauti wakilaani kitendo alichofanyiwa Dk Ulimboka.

Dk Chitega alisema hadi kufikia jana, walikuwa wamepata fedha zilizokuwa zikihitajika kwa ajili ya matibabu yake. Juzi madaktari hao walisema wanahitaji Dola za Marekani 40,000 (Sh63.2 milioni) ili kumtibu mwenzao nje ya nchi.


No comments: