Sunday, December 30, 2012

CHADEMA: Piga Ua garagaza Ni Dk. Slaa tena Mwaka 2015

Dr. Willibrod Slaa, Generalsekretär der CHADEM...
Dr Wilbroad Slaa


 CHAMA  cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetangaza kuwa Katibu Mkuu wake, Dk Willbrod Slaa atapewa fursa ya kuwania nafasi ya Urais kwenye uchaguzi mkuu ujao, mwaka 2015.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alitangaza hatua hiyo jana, alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Mpira, mjini Karatu mkoani Arusha, huku yeye akijiweka kando kuwania nafasi hiyo.

Hata hivyo, Dk Slaa mwenyewe alipoulizwa iwapo ana nia ya kugombea urais mwaka 2015, alisema: “Kwani mwaka 2010 nilijitangaza mwenyewe?, Iwapo wanachama wa Chadema watanipendekeza, nitafikiria kufanya hivyo.”



Katika maelezo yake Mbowe alisema: “Kama Mwenyezi Mungu atampa uhai na afya njema hadi mwaka 2015, Dk Slaa anatosha na Chadema, tutampa fursa nyingine ya kupeperusha bendera ya chama kwenye nafasi ya urais.”
Huku akishangiliwa na umati wa wana chama wa Chadema Mbowe aliongeza: “Ninataka wanaotumia ugombea Urais kama kete ya kuleta mtafaruku ndani ya Chadema watambue hivyo.”

Alibainisha kuwa, binafsi hana nia ya kuwania urais na badala yake atatumia nguvu, uwezo na kila kilicho ndani ya uwezo wake, kukijenga Chadema ili kushinde uchaguzi na kushika dola.

Mbowe alisema kwa muda mrefu kumekuwapo mbinu na jitihada za kumgombanisha yeye na Dk Slaa kuhusu nafasi ya urais na kutamba kwamba njama hizo kamwe hazitafanikiwa.
Mwenyekiti huyo wa Chadema alitumia pia mkutano huo kutangaza kumalizika kwa mgogoro uliokuwapo kati ya viongozi wa chama hicho wilayani Karatu.

Hata hivyo, awali katika mahojiano maalumu na gazeti hili, Mbowe alisema: “ Kikao cha CC (Kamati Kuu), kitakachofanyika Januari mwakani ndicho kitakachoweka utaratibu rasmi wa watu wanaotaka kuwania kiti cha udiwani, ubunge na urais mwaka 2015 na kutangaza nia zao na vigezo vya uteuzi.”

Alisema chama hicho kinakusudia kuwapa nafasi wenye nia kujitokeza mapema, ili kutoa fursa ya kuwaelewa, kuwaandaa, kuwapa mafunzo, kuwaeleza majukumu na wajibu wao, kuwaeleza sera, misimamo na malengo ya chama hicho.

Mbowe alisema kuwa mpango huo utakihakikishia Chadema wagombea wenye uwezo na uhakika wa kushinda mwaka 2015.
“Nia ya mpango huu ni kuepuka watu wanaodandia kuomba uteuzi wa kugombea dakika za mwisho,” alisema Mbowe.
Aliweka wazi kuwa chama hicho kitakuwa makini katika uteuzi wa nafasi ya urais kwa sababu ni nafasi nyeti, isiyohitaji kujaribu wala mzaha.

Alisema kwamba chama hicho hakitasubiri wala kupokea waliokosa fursa za uteuzi katika vyama vingine, kikiwemo Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambao wanaokimbilia Chadema dakika za mwisho akisema kuwa uzoefu umeonyesha wengi wao wanaendelea kuwa mamluki.
Alibainisha kuwa pamoja na vigezo vyote, wagombea hao pia watapimwa kwa uwezo wa kukijenga chama na kujituma, huku akionya kuwa watakaojitokeza kutangaza nia ya kugombea nafasi yoyote, lazima watambue kuwa mmoja pekee ndiye atakayeteuliwa kupeperusha bendera ya chama hicho.

Wakati Mbowe akitangaza hatua hiyo, Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa, amesema kuwa mwanachama yeyote wa chama hicho kikuu cha upinzani ana uhuru wa kutangaza nia ya kugombea nafasi yoyote ya uongozi.

Dk Slaa amesema hayo wakati umebakia mwaka mmoja kabla ya taifa kuingia kwenye uchaguzi wa Serikali za mitaa, vijiji na vitongoji huku pia ikisalia miaka miwili kabla ya kufanyika uchaguzi wa mkuu wa rais, wabunge na madiwani.

Kiongozi huyo wa chama hicho kikuu cha upinzani nchini, alitoa kauli hiyo jana katika mahojiano maalumu na Mwananchi Jumapili.

Ingawa awali suala la kutangaza nia ya kuwania nafasi mbalimbali hasa kiti cha urais ndani ya chama hicho lilizua mgogoro, lakini jana Dk Slaa alisema kuwa mwanachama yeyote anao uhuru wa kufanya hivyo na kwamba hakuna vipengele vya katiba vinavyomzuia.
“Katiba ya Chadema inatoa uhuru kwa mwanachama kutangaza nia ya kugombea nafasi yoyote. Hakuna sehemu yoyote inayoeleza atangaze wakati gani. Hivyo, yuko huru kutangaza nia wakati wowote,” alisema Dk Slaa.

Kauli za Dk Slaa na Mbowe, zimekuja wakati chama hicho kukiwa na msuguano ndani ya chama hicho kuhusu wanachama walioamua kutangaza nia ya kuwania nafasi mbalimbali za uongozi wa nchi kupitia chama hicho.

Pia zimekuja wakati tayari Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Taifa (Bavicha), John Heche amemtangaza Dk Slaa kuwa ndiye mgombea urais wa chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao mwaka 2015.
Mwaka 2010, Dk Slaa aligombea nafasi hiyo na kuibuka mshindi wa pili kwa kupata asilimia 26.34 nyuma ya Rais Kikwete ambaye alipata asilimia 61.17.

Aidha, tayari Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, naye ametangaza kuwa hakuna kitakachomzuia kuwania urais mwaka 2015 kupitia chama hicho.
Hata hivyo, uamuzi huo wa Zitto, umekuwa ukipata upinzani kutoka kwa baadhi ya wanachama akiwamo Mwasisi ya chama hicho, Mzee Edwin Mtei, ambaye alionya kuwa kitendo cha kiongozi huyo kutangaza mapema nia ya kuwania urais, kinaweza kukigawa chama hicho.

Kauli ya Dk Slaa kuruhusu wanachama kutangaza nia ya kugombea uongozi kupitia chama hicho, inatafsiriwa na wachambuzi wa kisiasa kuwa ni mwarobaini wa mgogoro ambao ungeweza kujitokeza ndani ya chama hicho kama chama kingeendelea kukaa kimya.

Novemba mwaka huu Zitto wakati alikifanya mahojiano na mtandao wa Jamii Forum, alisema kuwa viongozi wa chama hicho walikutana mjini Morogoro hivi karibuni na kutengeneza utaratibu wa watu kutangaza nia wanapotaka kugombea nafasi yoyote ya uongozi.
“Nadhani huu ni uamuzi mzuri wa chama, maana watu wengine wana wasiwasi usio na msingi wowote kwamba kuwa na wagombea wengi kwenye chama ni kuvuruga chama,” alisema Zitto na kuongeza:
“Lakini watu haohao, wanashangilia kweli wakiona demokrasia inavyotekelezwa kwenye nchi nyingine kama Marekani.”

Alisema kuwa tatizo la Watanzania wanapenda kuona demokrasia inatekelezwa, lakini wao wanaogopa kuitekeleza, hivyo mwongozo kwa wagombea ambao waliupitisha mjini Morogoro, utasaidia chama hicho.

Hata hivyo, jana Dk Slaa alisema hakuna utaratibu maalumu uliowekwa na chama juu ya nia ya kutangaza kugombea nafasi mbalimbali, bali Katiba ya Chadema, ndiyo inapaswa kuchunguzwa inaeleza nini juu ya hilo.

Katika hatua nyingine, kwenye  mkutano wa hadhara mjini Karatu, Mbowe alitangaza kumalizika kwa mgogoro uliokuwapo ndani ya Chadema katika wilaya hiyo.

Alisema kuwa  migogoro na tofauti za kimtazamo na mawazo miongoni mwa viongozi na wanachama wa Chadema, Mbowe alisema ni ishara ya uhai na maendeleo yanayotokana na wengi kutaka fursa zinazotokana na uimara wa chama hicho.
“Muhimu ni chama kuwa na utaratibu na njia za kudhibiti na kuyatatua matatizo kupitia vikao halali vya chama kama tulivyofanya Karatu bila kuacha mipasuko ya kudumu na madhara kwa chama,” alisema Mbowe.

Hata hivyo, Mwenyekiti huyo alionya kuwa chama hicho hakitawavumilia viongozi na watakaoanzisha vurugu, mitafaruku na migogoro yao binafsi na kuyageuza kuwa ya chama na hivyo kuhatarisha mshikamano ndani ya chama akisema watu hao watafukuzwa.

Source: Mwananchi
Enhanced by Zemanta

No comments: