Wednesday, January 30, 2013

Serikali yasalimu amri kuhusu gesi yakubali madai ya raia Mtwara

Waziri Mkuu Mizengo Pinda
WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda amefanikiwa kutuliza jazba za wakazi wa Mkoa wa Mtwara baada ya kueleza jinsi watakavyonufaika na gesi itakayozalishwa mkoani humo kabla ya kusafirishwa kwa bomba hadi Dar es Salaam.

Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Joseph Simbakalia amewaomba radhi wananchi wa mkoa huo kutokana na kauli Desemba 21, mwaka jana akiwakebehi baada ya kumwomba apokee maandamano yao ya kupinga mpango wa kusafirisha gesi hiyo.



Akizungumza katika mkutano wa majumuisho uliofanyika jana baada ya kusikiliza madai ya wananchi hao kwa siku mbili mfululizo, Pinda alisema hakuna tone la gesi ghafi itakayosafirisha kwa njia ya bomba na kusema kiwanda cha kusindika gesi ghafi kitajengwa katika Kijiji cha Madimba, mkoani humo ili mabaki yatokanayo na gesi hiyo yatumike kuvutia uwekezaji wa viwanda.

“Wataalamu wanasema gesi haiwezi kwa namna yoyote ile kusafirishwa kama ilivyo, lazima ibadilishwe kuwa hewa au barafu… kiwanda cha kusafisha gesi kitajengwa Madimba. Gesi yote itakayotoka Mnazi Bay itasafishwa hapo na masalia yote yatabaki huku ili kuvutia viwanda vya mbolea na vingine vinavyotumia malighafi hizo,” alisema Pinda na kuongeza:
“Kama tungekuwa tunasafirisha gesi ghafi basi hata kiwanda cha Dangote kisingejengwa hapa… gesi itakayopelekwa Dar es Salaam ni ile iliyosafishwa kwa ajili ya matumizi ya kuzalisha umeme… tusaidieni wenzetu kuliokoa Taifa na tatizo la umeme.”
“Gesi lazima isindikwe Mtwara, haitoki hadi viwanda vije… nadhani hili ni jambo jema lazima tuliwekee utaratibu. Nikawauliza wataalamu wangu kwani kiwanda cha kusafisha gesi kinajengwa wapi, wakanijibu Madimba… nikasema kumbe tatizo kubwa ni kutowaeleza vya kutosha wananchi suala la gesi.” alisema Waziri Mkuu huku akipigiwa makofi... “Nafikiri tatizo ni sisi Serikali hatukuwa na mpango mzuri wa kuwaelimisha wananchi.”
A
wali, madai ya wakazi wa Mkoa wa Mtwara yalikuwa ku pinga usafirishaji wa gesi ghafi kwenda Dar es Salaam wakieleza kuwa mpango huo utafukuza uwekezaji wa viwanda mkoani humo ambao ungechochewa na upatikanaji wa malighafi baada ya kusafishwa kwa gesi.

Pia wananchi walipinga uje nzi wa mitambo ya kuzalisha umeme Kinyerezi, Dar es Salaam wakiitaka Serikali kujenga mitambo hiyo mkoani Mtwara.

Alitoa wito kwa wabunge wa Mkoa wa Mtwara kufuta tofauti zao za kisiasa ili waweze kuharakisha maendeleo ya mkoa huo... “Purukushani hizi ndani ya chama hazina tija, tuseme basi… wabunge hawaelewani, sasa bungeni wanakwendaje... kila mtu na lake … hebu tuseme watu kwanza mimi badaaye,” alisema Pinda huku akishangiliwa.

Katika siku hizo mbili mkoani Mtwara, Waziri Mkuu alikutana na viongozi wa vyama vya siasa, dini, wafanyabiashara, madiwani na wenyeviti wa mitaa na wanaharakati mbalimbali.

RC aomba radhi
Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa, Simbakalia aliwaomba radhi wakazi wa Mkoa wa Mtwara akisema alipotoka kuwaita wananchi hao wapuuzi na baadaye wahaini kauli ambazo ziliwaudhi wengi
“Kupitia hadhara hii nawaomba radhi kwa kuwakwaza, nimesikitishwa kwa kauli yangu ambayo imepokewa kwa hisia kwamba niliwadharau,” alisema Simbakalia.

Baadaye Waziri Mkuu aliwasihi wananchi wa Mtwara kumsamehe Mkuu wao wa Mkoa wa Mtwara kwa kauli hiyo aliyoitoa 21 Desemba, mwaka jana katika kikao cha Kamati ya Ushauri Mkoa, (RCC), pale alipoombwa kuyapokea maandamano ya wakazi wa mkoa huo Desemba, 27, mwaka jana.

Source: Mwananchi

No comments: