Friday, August 16, 2013

Ponda achomolewa hosptali apelekwa gerezeni Segerea



JESHI la Polisi limemwondoa hospitalini kimyakimya Katibu wa Taasisi na Jumuiya za Kiislam, Sheikh Ponda Isa Ponda, na kumpeleka katika gereza la Segerea bila ndugu zake kuwa na taarifa.


Ponda (54) ambaye kwa sasa anakabiliwa na kesi mpya ya kufanya uchochezi katika maeneo mbalimbali nchini alisomewa shtaka hilo juzi katika wodi ya Kitengo cha Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Upasuaji wa Mishipa ya Fahamu (MOI) alipokuwa akipatiwa matibabu.

Wakili wake, Nassor Jumaa,amesema kuwa amesikitishwa na hatua ya vyombo vya dola kumuondoa mteja wake asubuhi na kumhamishia gerezani.

Alisema kuwa amesikitishwa na kitendo hicho kwani Hakimu Hellen Riwa, muda mfupi baada ya wakili mwandamizi wa serikali, Tumaini Kweka, kumaliza kumsomea shtaka Ponda juzi, alitoa amri ya mteja wake kuendelea kukaa chini ya ulinzi.

“Wanausalama wamemtoa wodini na kumpeleka katika gereza la Segerea na sasa atalazimika kurudishwa tena mahakamani siku kesi yake itakapojatwa Agosti 28 mwaka huu.
“Kwa kweli kitendo hicho kimenisikitisha na kunishtua sana ila tunatafakari ni hatua gani za kisheria tutazichukua siku za usoni,” alisema.

Polisi wafafanua
Jeshi la Polisi nchini limetoa taarifa kuwa Sheikh Ponda anajulikana alikopelekwa na kukanusha uvumi kuwa hajulikani alikopelekwa.

Akizungumza na waandishi wa habari, msemaji mkuu wa jeshi hilo, Advera Senso, alisema wametimiza maelezo ya hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Katika hatua nyingine, Senso alisema wanamshikilia askari wake mmoja kwa tuhuma za kufyatua risasi hewani wakati wa purukushani za kurushiana mawe na wafuasi wa Sheikh Ponda wiki iliyopita mkoani Morogoro.
“Tayari timu imeanza kazi na inaendelea vizuri kufuatilia na kuchunguza hali halisi ilivyokuwa kabla na baada ya purukushani hizo zilizohusisha wafuasi wa Ponda kurusha mawe na polisi kufyatua risasi hewani,” alisema.
Senso alikanusha kuwa risasi iliyofyatuliwa siyo iliyomlenga Ponda, na kusisitiza kuwa kanuni na taratibu za jeshi zinaelekeza kwamba kutafunguliwa jalada la uchunguzi kwa askari yeyote anapofyatua risasi iwe ni bahati mbaya au katika mazingira yanayolazimu.

Katika hatua nyingine, Senso alisema kuwa Julai 30, mwaka huu, saa moja jioni maeneo ya Vingunguti majambazi sita yalikurupushwa na polisi na kutelekeza begi lao ambalo ndani lilikutwa na bomu la kurushwa kwa mkono lililotengenezwa nchini Urusi.

Alifafanua kuwa katika sakata hilo watuhumiwa wanne wanashikiliwa na polisi.
Watuhumiwa hao wanadaiwa kukutwa na bunduki yenye namba 11276, magazine yenye risasi 23 na kwamba jeshi linaendelea kumtafuta raia wa kigeni anayedhaniwa kuwa ni Mtutsi ambaye anadaiwa kuingiza mabomu hayo nchini.

Senso alisema wanachunguza bomu hilo kuona kama lina uhusiano wowote na mabomu yaliyolipuka mkoani Arusha.