Wednesday, May 4, 2011

Mauaji ya Osama bado ni gumzo duniani




Kiongozi wa kundi Al-Qaeda Osama Bin Laden hakuwa amejihami wakati alipouawa na majeshi ya Marekani siku ya jumapili baada ya kukataa kukamatwa, ikulu ya White House imesema.

Shirika la kijasusi la Marekani(CIA) limesema halikujulisha Pakistan kuhusu uvamizi huo kutokana na hofu kuwa huenda ingehatarisha operesheni yao.

Pakistan imekanusha ufahamu wa uvamizi huo na idara ya ujasusi wa nchi hiyo imesema imeaibika na kutofaulu kwao.

Maafisa wa Marekani wamesema bado hawajaamua lini watoe picha ''za kutisha'' za mwili wa Bin Laden.

Lakini mkurugenzi wa CIA Leon Panetta ameiambia kituo cha televisheni cha NBC nchini Marekani kuwa bila shaka picha ya mwili wake itatolewa wakati mmoja.

Msemaji wa ikulu ya White House Jay Carney amesema mke wa Bin Laden alipigwa risasi kwenye mguu wake lakini hakuuawa.

Jumapili iliyopita, ikulu ya White House ilisema mwanamke huyo aliuawa katika makabiliano baada ya Bin Laden kumtumia kama ngao.

Bin Laden, mwenye umri wa 54, alikuwa mwanzilishi na kiongozi wa kundi la al-Qaeda. Inaaminika aliamuru mashambulizi yaliyotokea mjini New York na Washington 11 Septemba 2001, pamoja na mashambulizi mengine ambapo watu waliuwawa.