Tuesday, July 5, 2011

Simba yaitafuna Bunamwaya yaingia nusu fainali

Yailaza 2 - 1 , Al Mereikh nayo yaingia nusu fainali

Hayawi hayawi hatimaye yamekuwa, Leo timu ya Simba ya Tanzania imeingia kwa kishindo hatua ya nusu fainali ya mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati maarufu Kagame Cup baada ya kuibamiza bila huruma timu ya Bunamwaya ya Uganda kwa jumla ya magoli 2 - 1

Walikuwa ni Simba walioanza kufunga goli katika kipindi cha kwanza ambapo mmoja wa wachezaji wa Bunamwaya kutumbukiza mpira wavuni alipojaribu kurudisha mpira kwa golikipa wake Hamza Muwonge .

Baadaye Bunamwaya nayo ikiajipatia goli na kufanya timu zote ziende mapumzika kila moja ikiwa na 1 - 1.

Kipindi cha pili kilikuwa kigumu ambapo kila timu ilikuwa ikijaribu bahati yake ni simba ndio walioweza kupata goli kupitia kwa Jery Santo katika dakika 83 na hivyo kuizamisha timu ya Bunamwaya.

Katika mchezo mwingine wa robo fainali uliochezwa katika uwanja huo huo wa Taifa mjini Dar es Salaam timu ya Al Mereikh ya Sudan nayo imeingia hatua ya nusu fainali ya Kagame Cup baada ya kuifunga timu ya Ulinzi ya Kenya mikwaju 9 kwa 8 baadaya dakika 90 za kawaida kutopata mshindi.

Hadi mpira unamalizika timu zote zilikuwa zimefungana 1 - 1.

Kesho katika uwanja huo huo wa Taifa wa Dar es Salaam timu ya St. George ya Ethiopia itaumana vikali na timu ya Vital'o ya Burundi katika mchezo wa kwanza wa robo fainali na baadae katika mchezo wa pili wa robo fainali timu ya Yanga ya Tanzania watapepetana vikali na timu ya Red Sea ya Eritrea.