Sunday, August 7, 2011

CHADEMA yatimua uanachama madiwani watano

Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe

Chama cha Demokrasia na maendeleo CHADEMA kimewafukuza uanachama wa chama hicho madiwani watano wa mkoa wa Arusha kwa kile kinachodaiwa ni kukiuka maamuzi ya kikao cha Kamati Kuu ya Chama hicho.

Taarifa kamili ya chama hicho hii hapa chini


CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA).TAARIFA KUHUSU MAAMUZI YA KAMATI KUU YA CHADEMA YALIYOFIKIWA KATIKA MKUTANO WA DHARURA ULIOFANYIKA SIKU YA JUMAMOSI/JUMAPILI TAREHE 06-07 AGOSTI 2011 KATIKA HOTELI YA IMAGI MJINI DODOMA

Kamati Kuu ya CHADEMA ilikutana katika Mkutano wa Dharura uliofanyika siku ya Jumamosi na Jumapili tarehe 06 Agosti 2011 katika Hoteli ya Imagi Mjini Dodoma.

 Pamoja na mambo mengine Ilifikia maamuzi yafuatayo :

 1. Kamati Kuu ilipokea taarifa ya utekelezaji wa maagizo iliyoyatoa katika Mkutano wake wa tarehe 17 Julai 2011 iliyowataka madiwani wa CHADEMA Arusha kujiuzulu nafasi walizozipata pamoja na kuomba radhi kwa makosa waliyoyafanya kutokana na mwafaka uliofikiwa baina yao na madiwani wenzao wa TLP na CCM kwa kuwa chama hakikuridhia wala kuutambua mwafaka huo.

2. Kamati Kuu imezingatia kuwa, kati ya madiwani 10 waliopewa maelekezo na Kamati Kuu, madiwani watano (5) ndio wametekeleza maelekezo kikamilifu wakati madiwani wengine watano (5) wamekataa kuyatekeleza maelekezo hayo.

3. Baada ya kutafakari kwa kina taarifa ya utekelezaji wa maagizo ya Kamati Kuu, na kuwapa nafasi ya kujieleza mbele ya Kamati Kuu Madiwani ambao walikuwa hawajatekeleza maelekezo,Kamati Kuu imezingatia kuwa madiwani wamekataa kutekeleza maagizo ya Kamati Kuu. Aidha, Kamati Kuu imezingatia kuwa kitendo cha madiwani kukataa kutekeleza maagizo halali ya Kamati Kuu ni utovu mkubwa wa nidhamu na ni kuvunja maadili na kanuni za chama, na kinaenda kinyume na msingi mama wa CHADEMA wa uwajibikaji.

Hivyo basi, kwa kutumia mamlaka ya Kikatiba Kamati Kuu imewafukuza uanachama madiwani watano wafuatao kwa kosa la kukataa kutekeleza maagizo ya Kamati Kuu:
i) Ndugu Estomih Mallah ii) Ndugu John Bayo iii) Ndugu Charles Mpanda iv) Ndugu Rehema Mohamed v) Ndugu Reuben Ngowi.

Watajwa hapo juu wamejulishwa maamuzi ya Kamati Kuu ndani ya Mkutano tarehe 07 Agosti 2011 saa 7:57 usiku, Aidha, kila mmoja wao atakabidhiwa barua yenye kueleza maamuzi ya Kamati Kuu.

4. Aidha, Kamati Kuu imepokea taarifa ya mazungumzo baina ya Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Mhe Freeman Mbowe, na Waziri Mkuu, Mhe Mizengo Pinda, juu ya nia na azima ya kumaliza tatizo la mgogoro wa umeya Arusha, waliyoyafanya asubuhi ya siku ya Jumamosi, Tarehe 06 Agosti 2011 nyumbani kwa Waziri Mkuu Mjini Dodoma. Kamati imezingatia kuwa:
  •  a. Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa na Waziri Mkuu wamekubaliana kuunda Kamati ya Kitaifa ya kushughulikia mgogoro wa umeya wa Arusha itakayojumuisha wajumbe kutoka sehemu mbili zinazohusika katika mgogoro huu ambazo ni CCM na CHADEMA.
  • b. Kamati ya Kitaifa ya Maridhiano itaundwa haraka iwezekanavyo, na kwa vyovyote mgogoro wa u meya Manispa ya Arusha ulikubalika uishe ndani ya mwezi mmoja tangu tarehe ya mazungumzo ya Mwenyekiti wa Taifa na Waziri Mkuu.  
  • c. Uenyekiti wa Kamati ya Kitaifa utakuwa chini ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Ndugu John Tendwa, na kwamba Msajili wa Vyama vya Siasa ataratibu uundwaji wa Kamati hiyo ya Kitaifa.  
5. Kamati Kuu imetambua juhudi za Waheshimiwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, na Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Mhe Freeman Mbowe, kwa hatua yao chanya ya kumaliza mgogoro wa Arusha.

6. Pamoja na hatua njema kuelekea kumaliza mgogoro wa umeya Arusha, Kamati Kuu ya CHADEMA itaendelea kusitisha kumtambua rasmi Meya wa Arusha hadi pale mazungumzo yaliyoanishwa hapo juu yatakapokamilika na mwafaka bayana kupatikana. Imetolewa na:

 ………………. Mhe. Freeman Aikaeli Mbowe (Mb)


No comments: