Thursday, November 29, 2012

UDOM yaanza Uchunguzi Kashfa ya Wanafunzi wa Kike kujiuza



Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udoso), imeanza kuchunguza tuhuma za baadhi ya wanafunzi kujihusisha na biashara ya ukahaba ili kuwachukulia hatua za kinidhamu.

 Udoso ilichukua hatua hiyo baada baadhi ya vyombo vya habari nchini kuripoti taarifa kuwa baadhi ya wanafunzi wa chuo hicho wanajihusisha na biashara hiyo ya ngono. Akizungumza na waandishi wa habari jana kwa niaba ya wanafunzi hao, Rais wa Udoso, Yunge Paul, alisema kuwa tayari kazi hiyo imeanza na watakaobainika watachukuliwa hatua za kinidhamu.



Alisema kuwa watu hao wanashusha heshima ya chuo hicho kikubwa na kama taasisi ambayo imebeba wasomi wengi na ni kioo cha jamii. Aidha, alisema taarifa hiyo ya kashfa ya ngono iliyoripotiwa na vyombo vya habari imesononesha nchi nzima ukiwamo uongozi wa chuo.
 “Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari kwa kweli imesononesha nchi nzima ikiwamo Udom yenyewe na wanafunzi na hivyo kuwajengea mashaka hata waajiri wao ambao wanatambua wapo hapo kwa ajili ya kusoma,” alisema.

 Aliwaomba waandishi wa habari kushirikiana na taasisi hiyo katika kuhakikisha wale wote wanaojihusisha na biashara hiyo wanabainika.

 Wiki iliyopita kituo kimoja na televisheni kilionyesha picha za baadhi ya wasichana wanaodaiwa kuwa ni wanafunzi wa chuo hicho wakifanya biashara hiyo katika moja ya mitaa ya mjini Dodoma.

Pia katika mahojiano hayo, baadhi ya wanafunzi walionyesha kusikitishwa na vitendo hivyo na kuongeza kuwa vinawadhalilisha.

 Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idrissa Kikula, alikaririwa akisema ni vigumu kuwabaini wanafunzi wanaojihusisha na biashara. Alisema watatumia Jeshi la Polisi kuwabaini wanafunzi hao ili wachukuliwe hatua.

Source: IPP Media