Thursday, December 6, 2012

"Sijawahi kuzini, Kipimo cha DNA kimesema Mtoto si wa Ndoa, Nimepewa Talaka!!!"



MWANAMKE mmoja mkazi  Ilala, ameibuka na kukishutumu kipimo cha vinasaba (DNA) cha kutambua uhalali wa baba kwa mtoto, kwamba hakina ukweli kwani kimevunja ndoa yake.
Frederica Michael alikosoa kipimo hicho kuwa kina upungufu mkubwa, kwani hakikutoa majibu ya ukweli katika kesi ya  uhalali wa mtoto wake mwaka 2005.

Alisema mwaka 2005, familia hiyo ilikwenda kupima kujua iwapo mtoto wao  aliyezaliwa mwaka 2004, ni mtoto halali wa mume wake, Constatine Moshi.
“Nimejifungua Aprili 11, 2004 wakati huo mume wangu alikuwa safarini, aliporudi na kumkuta mtoto alibadilika na kusema siyo wake,” alisema Michael.



Alisema mume wake alikuwa akimtuhumu kuwa, ana uhusiano na bosi wake jambo ambalo mwanamke huyo alilikanusha vikali.
Wiki hii gazeti la Mwananchi lilitoa takwimu za mwaka huu za matokeo ya vipimo vya DNA kutoka maabara ya Mkemia Mkuu, ambazo zinaonyesha asilimia 44  ya waliokwenda kupima uhalali wa baba  siyo wazazi halisi wa watoto hao.

Mwanamke huyo alisema  mume  wake, alimkataa mtoto huyo akidai ana asili ya Kiarabu jambo ambalo Michael alilikataa na kudai kuwa, ukoo wao ni weupe na wana nywele laini hivyo yawezekana amerithi upande huo.

Alisema mgogoro huo ulikua na mwaka 2005, waliamua kupima DNA  na Julai 20, mwaka huo huo majibu yalitoka yakionyesha mtoto huyo siyo halali wa Constatine.
Michael anakanusha vikali majibu hayo, akisema yana upungufu mkubwa kwani yeye ndiye anayeujua ukweli.
“Sikuwahi kuzini nje ya ndoa tangu nimefunga ndoa mwaka 1999 na mume wangu Mushi ambaye nimezaa naye watoto saba,” alisema.

Alisema kipimo hicho kinatekelezwa na wanadamu,  hivyo wanaweza kufanya makosa ambayo yameigharimu ndoa yake.
‘Nilimpenda mno mume wangu Mushi, Mungu anajua, lakini ameniacha kwa sababu ya majibu ya DNA ambayo nina hakika yalifanyiwa hujuma au yalikosewa katika mikono ya binadamu,” alisema mwanamke huyo kwa uchungu.
Alisema ni vyema DNA kitumike kwa uangalifu kwani kinaweza kusababisha migogoro zaidi katika jamii.
Hata hivyo, Mkemia Mwandamizi wa Kitengo cha Masuala ya Jinai, Baiolojia na DNA, Gloria Machuve alisema kipimo hicho ni sahihi na kinatoa matokeo yenye ukweli kwa asilimia 99.
 Machuve alisema maabara hiyo ilinunua mitambo bora zaidi na kisasa, ili kupata matokeo yenye  uhakika hivyo matokeo yake  yana  uhakika na ukweli.

Source:Mwananchi

No comments: