Monday, March 18, 2013

Polisi yafanya upekuzi CHADEMA waondoka na nyaraka



Polisi imefanya upekuzi katika ofisi za makao makuu ya chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA na kuondoka na nyaraka mbalimbali kwa ajili kupata ushahidi zaidi kuhusu tuhuma zinazomkabili Afisa wa chama hicho Wilfred Lwakatare ambaye alikamatwa na polisi kwa tuhuma za kupanga njama za kuwadhuru baadhi ya watu wakiwemo waandishi.

Tukio hilo lilitokea jana ikiwa ni mwendelezo wa upelelezi wa tuhuma zinazomkabili Lwakatare ambazo zinazomhusisha na picha ya video iliyorushwa kwenye mitandao ya kijamii. Lwakatare alikamatwa Jumatano iliyopita akihusishwa na picha hiyo iliyomwonyesha Lwakatare akiwaelekeza watu ambao hawakuonekana, kufanya vitendo vya uvunjifu wa amani au uhalifu.
Upekuzi katika ofisi
Polisi hao wakiwa na Lwakatare na mmoja wa mawakili wake, Nyaronyo Kicheere walikwenda kwenye ofisi za Chadema saa 9.00 alasiri kwa ajili ya kufanya upekuzi.

Upekuzi huo uliendeshwa zaidi kwenye ofisi za Lwakatare kwenye Makao Makuu ya Chadema yaliyoko Mtaa wa Ufipa, Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Upelelezi wa kesi hiyo unaongozwa na Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Obadia Jonas. Uchunguzi wa gazeti hili unaonyesha kuwa upekuzi huo ulikuwa na lengo la kupata hati zenye mwandiko wa Lwakatare ili kufananisha na nyaraka mbalimbali walizonazo polisi. Kwa nyakati tofauti, Nyaronyo Kicheere na Ofisa Habari Mwandamizi wa Chadema, Tumaini Makene walithibitisha juu ya upekuzi huo.
Kicheere alisema aliitwa jana kwenda Kituo Kikuu cha Polisi, alipofika alielekezwa kufuatana na mteja wake na polisi kwenda Makao Makuu ya Chadema.
“Walifanya upekuzi kusaka nyaraka kwa ajili ya kuongeza ushahidi wa uchunguzi wao,” alisema Kicheere.
Naye Makene alikiri kufanyika kwa upekuzi na kufafanua ulifanyika ndani ya ofisi za Chadema.
Lwakatare kufikishwa mahakamani
Pia kwa nyakati tofauti Kaimu Mkurugenzi wa Upelelezi, Isaiah Mungulu na Msemaji wa Polisi, Advera Senso waliithibitishia Mwananchi kuwa Lwakatare atapandishwa kizimbani leo.
“Upelelezi umekwenda vizuri na kesho (leo) atapandishwa kizimbani ili kujibu mashtaka yanayomkabili,” alisema Mungulu.
Alipoulizwa kuhusu kupekuliwa kwa ofisi za Chadema jana alasiri, Mungulu alijibu suala hilo lilikuwa la kiufundi zaidi.
“Hilo suala ni `technical’ (kiufundi). Hilo siwezi kukujibu bwana,” aliongeza Mungullu.
Senso alisema kuwa upelelezi ulikuwa kwenye hatua nzuri na alithibitisha kuwa walimwita Kicheere kwa mahojiano zaidi kuhusu mteja wake.
“Tumemwita tena leo (jana) Wakili wa Lwakatare kama mwendelezo wa upelelezi wetu, suala hili linatakiwa lifanyiwe uchunguzi wa kina kwa hiyo siyo vibaya kumwita mara kwa mara,” alisema Senso.
Lwakatare alikamatwa saa saba mchana Machi 13, mwaka huu katika makao makuu ya chama hicho Kinondoni, ambapo alipelekwa katika Makao Makuu ya Polisi kwa mahojiano na baadaye kushikiliwa katika Kituo Kikuu jijini Dar es Salaam.  

Source: Mwananchi

No comments: