Sunday, May 8, 2011

Marekani yaanza kuonyesha picha za Osama



Marekani imeanza kuonyesha picha zinazomwonyesha aliyekuwa mtuhumiwa wa ugaidi namba moja duniani marehemu Osama bin Laden.

Tayari imeshaonyesha picha zipatazo tano za video zinazomwonyesha Osama kwenye jumba alimouawa hivi karibuni lililopo kaskazini mwa Pakstani akifanya shughuli mbali mbali.

Maafisa wa Marekani wanaamini jengo hilo alilitumia kama kituo cha kuratibu ugaidi duniani.

Katika picha hizo za video Osama anaonekana akiangalia mkanda wa video ukitangaza habari zinazomhusu na pia akifanya mazoezi ya kuhutubia kwenye runinga.

Katika video mojawapo Osama anaonekana akiangalia habari yenye ujumbe unaoelekezwa kwa raia wa Marekani "ujumbe kwa raia wa Marekani" amenukuliwa afisa usalama akisema.

Inaaminika picha hiyo ya video iliandaliwa mapema mwenzi Octoba na mwanzo mwa mwezi Novemba mwaka 2010.

Maafisa usalama wanasema alibadili ndevu zake zilizokuwa nyeusi wakati akirekodi mkanda huo na akaonekana akiwa na ndevu nyeupe wakati akiungalia mkanda huo yeye mwenyewe na hiyo inaamanisha alikuwa ni mtu aliyekuwa akijihadhari na kujaribu kuficha sura yake.

Picha hizo zote zinaelezwa zimepatikana kwenye jumba lake hilo ikiwa ni pamoja na vifaa ya digitali vya kurekodi sauti mafaili ya sauti na picha za video pamoja na nyaraka mbali mbali. Pia kumepatikana komputa vifaa vya kurekodia na nyaraka zilizoandikwa kwa mkono.

Zipo pia barua alizokuwa akiwasiliana na wenzake. Katika picha za video zilizoonyeshwa Osama anaonekana ameanza kuzeeka akiwa amekaa chini ya sakafu kwenye chumba chake akiwa amejifunika blanketi akiangalia runinga.