Sunday, January 27, 2013

Mtwara hapakaliki, Wanane wauawa kwenye vurugu





WATU wanane wameuawa na wengine kumi na moja kujeruhiwa kutokana na vurugu zilizizotokea jana mkoani Mtwara na Itete wilayani Ulanga, mkoani Mororgoro.

Muuguzi wa zamu katika Hospitali ya Wilaya ya Masasi, Mkomaindo, Amima Simbo alithibitisha vifo vya watu saba waliofikishwa hospitalini hapo.

Kwa mujibu wa muuguzi huyo, maiti zilizopokelewa hospitalini hapo zilionekana zikiwa na matundu yanayodhaniwa kuwa ni ya risasi, baadhi yao kichwani, begani, viunoni na tumboni.



Aidha majeruhi waliofikishwa hospitalini hapo pia walikuwa na majeraha mbalimbali ikiwamo ya risari.
Habari zaidi zinaeleza kuwa vurugu hizo zilizuka baada ya kundi la waandamaji, wengi wakiwa vijana waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda waliokuwa wakipinga mwenzao kukamatwa na kutaka kuvamia Kituo cha Polisi ili kumwokoa.

Vurugu hizo ziliendelea kuutikisa Mkoa wa Mtwara kwa siku ya pili mfululizo na kuutikisa Mkoa wa Mtwara, baada ya vurugu nyingine kuibuka wilayani Masasi jana.

Habari zinasema mbali na vifo na majeruhi, nyumba za wabunge wawili wa wilaya hiyo zimechomwa moto, ambapo pia magari, trekta, Ofisi za CCM Wilaya na Ofisi ya Mkurugenzi wa Wilaya ziliharibiwa kwa kuchomwa moto.

Wabunge ambao nyumba zao zimemwa moto ni Mariam Kasembe wa Masasi Mjini na Anna Abdallah Mbunge wa Viti Maalumu wilayani humo.

Juzi vurugu hizo zilitokea katika Mikoa ya Morogoro kati ya wakulima na wafugaji na kusababisha kifo cha mtu mmoja wakati mkoani Mtwara wananchi  wa eneo la Chikongola waliizingira nyumba ya diwani wa Kata ya Mikindani, Mohamedi Chehako kwa madai ya kuwahifadhi wachawi ndani ya nyumba yake.

Katika vurugu hizo polisi walilazimika kutumia silaha yakiwamo mabomu ya machozi ili kupoza hali ya hewa, ambapo nyumba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia ilichomwa moto.

Akizungumzia kuhusu vurugu hizo, Mbunge wa Masasi Mjini, Mariam Kasembe alisema kuwa nyumba yake iliyoko Masasi mjini imechomwa moto na kuteketea kabisa, huku mali zikiibwa na kwamba familia yake sasa haina makazi.

Aliongeza kwamba mbali na uharibifu, vurugu hizo zimesababisha pia mama yake mzazi kukimbia na mpaka sasa hajulikani alipo.
“Wamechoma trekta na gari lililokuwepo nyumbani kwangu, watoto wangu na mume wangu walipoona hali hiyo wakakimbia,” alisema Kasembe akieleza kuwa hawezi kuthibitisha chanzo cha vurugu hizo, lakini anahisi kuwa zinatokana na mgogoro wa gesi.

Alifafanua kwamba watu hao walifanya uharibifu huo baada ya kupanga njama huku wengine wakiwa wamekizingira Kituo cha Polisi, ili kuwazuia wasiende kuisaidia familia yake.
“Ofisi ya Bunge ilitaka kunisafirisha ili nikaangalie hali ilivyo, lakini wapigakura wangu na ndugu wameniambia nisiende ili kulinda usalama wangu,” alisema.

Naye Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Anna Abdalla alisema nyumba yake iliyopo eneo la Masasi mjini imechomwa moto katika vurugu zilizotokea jana.
“Ni kweli nyumba yangu nimesikia imechomwa moto, lakini sijui kinachoendelea,” alisema.

Mkazi wa Kijiji cha Chikunja, alipozaliwa Kasembe, Anna Martin aliliambia gazeti hili kuwa kundi jingine la vijana lipo katika harakati za kutaka kuichoma nyumba ya mbunge huyo, hali iliyosababisha wanafamilia wa mbunge huyo kutoka nje.

Shuhuda mwingine wa tukio hilo, Idi Mkwachu, ambaye ni Mkandarasi wa Wilaya hiyo alisema kuwa vurugu hizo zilianza saa mbili asubuhi jana, ambapo kundi la watu lililokuwa likizunguka mitaani lilikuwa  likiimba nyimbo za kuitaka Serikali ilipatie ufumbuzi suala la gesi.

Mkwachu alisema kuwa suala la gesi limezua uadui mkubwa kati ya wananchi na Serikali huku akidai kuwa kuna siri imebainika kuwa wabunge wanaoshinikiza gesi itoke Mtwara, wamepewa mamilioni ya fedha na Serikali.
“Kwa mfano gridi ya taifa ingeanzia Mtwara ingekuwa ni karibu zaidi kuliko gridi hiyo kujengwa katika eneo jingine. Mbona  kujenga bomba ni gharama kuliko gridi hiyo?,” alisema Mkwachu.

Alisema kwamba Serikali inavyochukua muda mrefu kutoa suluhu ya mgogoro huo, inajipalia makaa kwa sababu mikoa ya Mtwara na Lindi imebobea katika umaskini kwa miaka mingi.

Mkwachu alisema kuwa hadi kufikia jana saa kumi jioni, baadhi ya majengo yalikuwa yakiendelea kuteketea kwa moto, huku askari kutoka Nanyumbu na Nachingwea wakiletwa ili kusaidia kutuliza ghasia hizo.

Maaskofu watoa tamko
Wakati hayo yakiendelea, Baraza  la Maaskofu wa Makanisa ya Kipentekoste (PCT) Mkoani Mtwara, limetoa tamko likiitaka  Serikali isitishe mpango wake wa kusafirisha  gesi  kutoka Kijiji cha Msimbati mkoani humo, kwenda Kinyerezi Dar es Salaam.

Tamko hilo limetolewa jana na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Charles Chilumba walipozungumza na waandishi wa habari katika klabu ya waandishi wa habari Mtwara (MTPC), iliyopo mjini humo.

Chilumba alisema kuwa Serikali inatakiwa kuwa sikivu na kusikia kilio cha wananchi wa Mikoa ya Kusini  ya Lindi na Mtwara, ambako vyanzo vya uchumi wa gesi vipo ili kutekeleza madai yao.

Alisema kuwa, viwanda vya mbolea, plastic na saruji ambavyo viliahidiwa kujengwa, vijengwe sasa na zisiwe propaganda za kisiasa kutoka kwa viongozi wa Serikali, ili  kuondoa dhana iliyokuwapo miaka ya nyuma kuwa kusini ni  ukanda wa vita, hivyo hakuna sababu ya kuendelezwa.
“Serikali isisikilize wabunge wadanganyifu, ambao hawana makubaliano na wananchi katika majimbo wanayotoka, ambao huchochea mgogoro huu kwa lengo lao na masilahi yao binafsi,”alisema Chilumba.
”Inabidi wawaombe radhi bila masharti kwani semi zao  zinaleta chuki, uhasama, utengano katika nchi na kusababisha nchi isitawalike. Serikali ya CCM itekeleze Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2010 Ibara ya 63 kifungu H na K,”alisema.

Source: Mwananchi

No comments: