Monday, July 15, 2013

CHADEMA yazoa viti vyote vya udiwani Arusha, CCM chali!


Uchaguzi mdogo wa udiniwani umefanyika mkoani Arusha katika kata nne hapo jana kwa amani na utulivu huku matokeo  yakionyesha Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA kikizoa udiwani wa kata zote nne. 


Katika Kata ya Elerai, mgombea wa CHADEMA Injinia Jeremia Mpinga alimbwaga Emanueli Laizer wa CCM kwa kura 1,715, dhidi ya 1,239.

Kata hiyo ilikuwa na wapiga kura 23,797 waliojiandikisha na vituo 55 vya kupigia kura, lakini idadi kubwa ya wananchi hawakujitokeza.


Matokeo ya kura yalitangazwa chini ya ulinzi mkali wa askari polisi zaidi ya 40 wenye silaha, na kupokelewa kwa shangwe kubwa na wafuasi na mashabiki wa CHADEMA.

Katika Kata ya Kaloleni, mgombea wa CHADEMA, Kessy Emmanuel Miliare alimshinda kwa mbali mgombea wa CCM kwa kura 1,470 dhidi ya 530, wakati mgombea wa CUF ameambulia kura 275. waliojiandikisha 12,674 waliopiga kura 2,292. Kura halali ni 2,277 na zilizoharibika 15.

Akitangaza matokeo katika Kata ya Themi, Msimamizi wa Uchaguzi, Editha Mboye alimtangaza mgombea udiwani wa CHADEMA, Mallance Kinabo kuwa mshindi kwa kupata kura 678, akimwacha mbali mgombea wa CCM Victor Mkolwe aliyepata kura 326, huku yule wa CUF, Lebora Ndervai akipata kura 313.

Kata ya Kimandolu, CHADEMA pia wameibuka na ushindi mkubwa na kuiacha vibaya CCM.
Mgombea wa CHADEMA, Elishadai Ngowi amemshinda mgombea wa CCM, Edina Sauli kwa kura 2,265, dhidi ya 1,169 za mpinzani wake.

Mara baada ya kutangazwa kwa matokeo hayo, Jiji la Arusha lilizizima kwa shangwe na nderemo, huku idadi kubwa ya watu wakijipongeza kwa ushindi huo mkubwa.

Mwigulu Nchemba atimua
Matokeo hayo ambayo yameonekana kuwasononesha viongozi na wanachama wa CCM, yalimfanya Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Mwigulu Nchemba, kuondoka kimya kimya jijini hapa kwa kutumia gari maalumu.

Mwigulu ambaye aliongoza kikosi cha CCM katika kampeni za kimya kimya, majira ya jioni alionekana akielekea Moshi, huku wasaidizi wake wakiwemo wabunge wakitoweka katika vituo vya kuhesabia kura.

Mapema, wabunge wa CHADEMA na wa CCM tangu asubuhi walikuwa wakizunguka katika kata hizo, huku Mbunge wa Viti Maalumu, Catherin Mgige (CCM) akitumia gari ndogo, Salon yenye vioo vya giza alionekana akizunguka kata zote jana.

Ulinzi mkali wa polisi
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatusi Sabas jana aliongoza kazi ya ulinzi uliokuwa na idadi kubwa ya askari polisi wenye silaha za moto na mabomu ya machozi.

Akitumia gari aina ya Toyota Land Cruiser yenye namba TP 1715, Kamanda Sabas alionekana akizunguka katika mitaa ya kata zote nne, zilizokuwa zimesheheni idadi kubwa ya askari, wengi kutoka mkoani Kilimanjaro.

Waangalizi wa kimataifa
Katika tukio la kwanza la kihistoria, uchaguzi wa kata hizo ulishuhudiwa na waangalizi wa kimataifa kutoka taasisi ya International Low and Policy Institute yenye makao makuu yake nchini Norway, na wale wa ndani kutoka Jukwaa la Katiba.

Kiongozi wa waangalizi kutoka Norway, Sterling Roop, akiongea na Tanzania Daima alisema kuwa idadi ndogo ya wapiga kura imejitokeza na uwepo wa dosari kadhaa umewafanya baadhi ya wananchi kukosa haki yao ya kupiga kura.

Roop alisema pamoja na wananchi kuwa na shahada halali za kupigia kura na majina yao kuwepo, lakini hakukuwa na picha zao katika daftari la wapiga kura na hivyo wakazuiwa kupiga kura.

Katika vituo vingi, hususani Kata ya Kaloleni dosari kuu ilikuwa ni kukosekana kwa majina katika daftari la kupiga kura kwa wananchi ambao wana shahada na pia majina yao kubandikwa katika ofisi za kata kama wapiga kura halali.

Majina ya wapiga kura yatoweka
Dosari kubwa iliwakumba wapiga kura baada ya majina, picha na maelezo kukosekana kwenye daftari la wapiga kura karibu katika kata zote.

Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Hamid M Hamid alikiri tatizo hilo na kudai kwamba tayari alishawasiliana na wataalamu wake wa mifumo ya kompyuta (IT) ili washughulikie kasoro hizo kwenye kila kata iliyokuwa ikiendelea na uchaguzi.

Hata hivyo, alisema kuwa yeye si mchawi kuweza kubaini chanzo cha hitilafu hizo zilizojitokeza. Baadhi ya upungufu uliobainika ni baadhi ya watu kuandikishwa zaidi ya mara moja.

Kata ya Kaloleni kwenye kituo cha AICC Nursery B, mpiga kura Michael Laurence alikuwa ameandikishwa mara tatu kwenye daftari la wapiga kura akiwa na namba 48674955, 444666858 na 13142914.

Hata hivyo kwenye majira ya saa saba mchana, wataalamu wa kompyuta wa Tume ya Uchaguzi walifika na kuanza kuwasaidia wananchi waliokuwa wamejazana kwenye kituo cha kata hiyo.

Mmoja wa wataalamu hao, Siif Mtezo aliwaeleza waandishi wa habari kuwa tatizo hilo lilisababishwa na watu kujiandikisha zaidi ya mara moja.

Alisema kilichowafanya wengi washindwe kuona majina yao ni hofu kama ile inayowakumba wanafunzi wanaoenda kuangalia matokeo, na kwamba tume ililazimika kuwapigia simu wananchi wengi waliokuwa wameondoka, na wakarudi kupiga kura.

Wakala wa Chama cha Wananchi (CUF), Malik Abbas kwenye kituo hicho aliwaeleza waandishi wa habari kuwa wananchi wengi walifika, lakini majina yao hayakuonekana na wakaondoka, huku akionyesha baadhi ya picha ambazo hazionekani vizuri kutokana na kufifia kwenye daftari hilo.

Mgombea udiwani wa kata hiyo kwa tiketi ya CUF, Abbas Darwesh alisema wananchi wengi walishindwa kupiga kura akiwemo mtoto wake Omary Othman ambaye pamoja na kuwa na kitambulisho chake namba 32479962 jina lake halikuonekana kwenye orodha.
“Inawezekana kweli kuna mchezo mchafu umefanyika kubadili daftari la wapiga kura kama ambavyo tetesi zilikuwa zimezagaa, kwa sababu mtoto wangu mwenyewe alipiga kura kwenye kituo hiki katika uchaguzi wa 2010, lakini leo naambiwa jina lake halipo,” alilalamika Darwesh.

Msimamizi wa uchaguzi Kata ya Kaloleni, Anna Lebisa amekiri kukosekana kwa majina ya wananchi katika daftari licha ya kuwepo katika mbao za matangazo na kusema hawakuruhusiwa kupiga kura.

Miongoni mwa waliokumbwa na kadhia hiyo ni Omari Othmani na mtangazaji wa TBC, Khalifa Mshana ambaye alilazimika kulifikisha suala lao kwa Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji mstaafu Hamid Mahmood ambaye alimuachia ofisa wa tume kulishughulikia.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba, Deus Kibamba akiwa na timu yake ya waangalizi wa uchaguzi huo, alisema kura zimeanza kupigwa taratibu na idadi ndogo ya watu kujitokeza akidai kumechangiwa na hofu kubwa baada ya kuwepo kwa askari wengi katika vituo vya kupigia kura.
“Wingi wa askari wenye silaha za moto katika vituo vya kupigia kura umechangia kufanya baadhi ya wananchi kutojitokeza kwa hofu ya askari hao,’’ alisema Kibamba.

Wafuasi wa CHADEMA watekwa, wapigwa
Matukio ya kutekwa na kupigwa kwa wafuasi wa CHADEMA yalijiri katika uchaguzi huo jana.

Vijana wanaoaminika kuwa ni wa CCM, wakiwa ndani ya gari aina ya Land Cruiser iliyoegeshwa kwenye uwanja wa AICC wa Soweto waliwakamata na kuwapiga baadhi ya wananchi waliokuwa wakielekea katika vituo vya kupigia kura eneo la Soweto.

Msimamizi wa uchaguzi wa Kata ya Kaloleni, Lebisa alikiri kuliona gari hilo majira ya saa tatu asubuhi. Aliwaelekeza polisi waliokuwa kwenye kituo hicho kuwafuatilia, lakini waliondoka kabla hawajakamatwa.

Aidha, mwananchi mwingine, Hassan Noor ambaye alikuwa wakala wa CHADEMA kwenye kituo cha AICC Nursery alishindwa kufanya kazi hiyo baada ya kunyang’anywa barua yake na vijana waliokuwa kwenye gari aina ya Land Cruiser ya rangi ya maziwa ambayo namba zake hakuzishika.

Akiongozana na wenzake wawili kwenye mzunguko karibu na kituo hicho cha kupigia kura, Noor aliona gari hilo likisimama karibu yao na kuwataka waondoke eneo hilo. Aliwaeleza kuwa ni mawakala, ndipo walipomtaka awaonyeshe barua.
“Nilijua ni askari, na nilipowapa wakaninyang’anya na kuichana. Kisha wakampiga mwenzangu Boniface Kimaro. Alipigwa na kitu kama chuma kichwani na wakaondoka. Tumeripoti Kituo cha Kati cha Polisi,” alisema.

Katika Kata ya Kimandolu, watu sita walikamatwa wakiwa wamekaa katika gari moja na kupelekwa polisi kwa mahojiano, hali hiyo ikajitokeza tena katika Kata ya Kaloleni pia, ambako watu wasiojulikana walikamatwa wakiwa wamejificha ndani ya gari. 

Source: Tanzania Daima


No comments: